Timu ya Moro United ya mkoani Morogoro iliyokuwa inashiriki Ligi Kuu ya Tanzania Bara na kuleta upinzani katika mechi zake za ligi hiyo dhidi ya klabu kongwe za Simba na Yanga `imesambaratika`.
Kwa mujibu wa habari zilizopatikana jijini Dar es Salaam timu hiyo iliyokuwa inasimamiwa kazi zake za utendaji na baadhi ya wadau wa soka kutoka katika klabu za Simba na Yanga imeshindwa kuendesha zoezi la usajili wa wachezaji wake kwa ajili ya msimu ujao wa ligi kama ilivyotangazwa na Shirikisho la Soka Tanzania, TFF.
TFF ilipotangaza kuwa kila klabu inatakiwa kutangaza majina ya wachezaji wake inaowaacha na pia kabla ya Juni 15, Moro United hakuna mchezaji hata mmoja aliyetangazwa kuachwa na pia katika muda wa kufanya uhamisho klabu hiyo haikufanya chochote hadi muda huo ulipomalizika.
Na katika hali isiyo ya kawaida pia viongozi wa Moro United hadi jana pia walishindwa kupeleka majina ya wachezaji itakaowatumia katika msimu ujao ikiwa ni katika muda wa nyongeza baada ya Julai 15 kuwa ndio mwisho.
Hata hivyo habari ambazo Nipashe imezipata ni kwamba, viongozi watatu kutoka katika kundi la Friend\'s of Simba (majina tunayo) ndiyo wamejitokeza na kutaka kuichukua timu hiyo kwa lengo la kutaka kuiendesha.
Chanzo hicho kiliendelea kusema kuwa hata pale viongozi wa TFF walipokuwa wakiwasiliana na viongozi wa Moro United ambao walikuwa wakifanya kazi za timu hiyo kila mmoja alionekana kutokuwa na taarifa zozote za timu hiyo na kuelekeza atafutwe kiongozi mwingine.
Rais wa Moro United, Ismail Aden Rage ambaye huingia katika vikao mbalimbali vya soka akiiwakilisha timu hiyo aliliambia gazeti hili kuwa yeye hana taarifa zozote za timu na suala la usajili aliachiwa katibu wa timu, Hassani Maringo.