Meya wa Manispaa ya Dodoma, Bw. Francis Mazanda amesema watendaji wengi katika halmashauri nchini, si waaminifu bali ni wadanganyifu.
Pia amesema halmashauri nyingi hapa nchini, ni dhaifu katika kukusanya mapato huku baadhi ya watendaji wake kushindwa kujituma kikamilifu.
Aliyasema hayo wakati wa mdahalo wa `Ulingo wa Maendeleo` uliofanyika jana mjini hapa.
Mdahalo huo uliandaliwa na shirika lisilo la kiserikali la Asasi ya Kiraia, uliwashirikisha baadhi ya Wabunge na Wakuu wa Wilaya zote za mkoa wa Dodoma, wawakilishi mbalimbali wa asasi za kijamii na wakulima wa mkoani Dodoma.
Vile vile, alisema changamoto inazozikabili halmashauri nchini, ni pamoja na mawakala wake wanaotumika katika kukusanya kodi, kutokuwa waaminifu.
Hata hivyo, Bw. Mazanda alisema halmashauri nyingi zinakabiliwa na uhaba wa vitendea kazi.
Alisema tatizo lingine linalozikwaza halmashauri nchini, ni kuitegemea mno Serikali Kuu.
Kwa msingi huo, alizitaka kuacha utegemezi na badala yake kubuni na kutafuta vyanzo mbalimbali ili ziweze kupata mapato zaidi kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wake.Lengo la mdahalo huo lilikuwa ni kuwahamasisha wananchi ushiriki wao katika mchakato wa serikali za mitaa na Bunge.
Mbunge wa Dodoma Mjini, Bw. Ephraim Madege, aliwasilisha mada katika mdahalo huo kuhusu kazi za Bunge na Wabunge.
Wengine waliowasilisha mada katika mdahalo huo ni Bw. Andrew Komba ambayo ilihusu Mahusiano ya Wananchi, Bunge na Serikali za Mitaa katika mchakato wa maendeleo