PINDA: HATUOGOPI MAFISADI WA EPA, RICHMOND.
Habari Zinazoshabihiana
• Serikali yaahidi kuwachukulia hatua mafisadi 16.02.2008 [Soma]
• Nikichukua rushwa Mungu anichukue - Pinda 04.03.2008 [Soma]
• Pinda awageukia vigogo waliojilimbikizia mali 03.03.2008 [Soma]
*Asema anajua wananchi wana matarajio makubwa
*Asisitiza kusubiri uchunguzi kupata usahihi
*Alonga papara zinaweza kuifikisha nchi pabaya
Na Rashid Mkwinda, Njombe
WAZIRI Mkuu Bw. Mizengo Pinda, amesema Serikali haiogopi watuhumiwa wa ufisadi na wizi wa fedha za Richmond na EPA bali kinachofanyika ni kudumisha utawala bora kwa kufanya uchunguzi na kutenda haki kwa mujibu wa sheria za nchi.
Waziri Mkuu alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita, katika Kanisa la Anglikana mjini Njombe, Iringa, alikohudhuriwa kusimikwa kwa Askofu Mkuu wa Kanisa hilo Usharika wa South West Tanganyika, Dkt. John Simalenga.
Bw. Pinda alisema wananchi wana matarajio makubwa kwa Serikali yao, juu ya kupata matokeo ya taarifa sahihi za tuhuma za ufisadi na kwamba kinachofanyika ni uchunguzi wa kina ili kujiokoa na tatizo lililopo mbele.
Alisema hata kuingia kwake katika wadhifa alionao, kulitokana na mchakato wa tuhuma za ufisadi serikalini, hivyo ni wajibu wake kufanya kazi kwa uangalifu ili ipatikane haki kwa watuhumiwa.
"Naamini watu wana matarajio makubwa, bali tunafuata utawala wa sheria, tunafanya uchunguzi kwa umakini mkubwa, lengo letu ni kutenda haki na kujiokoa, vinginevyo hawa akina Jaji Augustine Ramadhani watatuhoji juu ya uamuzi wetu usiozingatia sheria," alisema huku akielekeza macho yake kwa Jaji Mkuu ambaye alikuwamo kanisani humo akipiga kinanda.
Akizungumzia tatizo la UKIMWI Bw. Pinda alisema mkoa wa Iringa kwa sasa unashika nafasi ya kwanza kwa maambukizi kwa asilimia 15.7 na kusababisha yatima 50,000 na kwamba 13,000 wapo wilayani Makete peke yake.
Aliwataka wananchi kuwa na tahadhari ya vitendo vya ngono huku akiwataka viongozi wa dini kutoa mafundisho sahihi juu ya tatizo hilo, ambapo pia alihimiza matumizi ya kinga kwa wale ambao watashindwa kujizuia na tamaa.
Awali Askofu Mokiwa aliitaka Serikali kuwataja wanaorejesha fedha za EPA ili kuondoa wasiwasi kwa wananchi.
Waziri Mkuu alikuwa katika ziara ya siku mbili katika mikoa ya Mbeya na Iringa ambapo katika mkoa wa Mbeya, aliendesha harambee ya uchangiaji wa Chuo Kikuu cha Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Konde, ambapo jumla ya sh. milioni 241.9 zilichangwa zikiwamo ahadi za sh. milioni 112.6.